JIDE VS KUSAGA...


MWANAMUZIKI Judith Wambura ‘Lady Jaydee’, juzi Jumatatu hatimaye yalimkuta baada ya kuibua simanzi nzito katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni, Dar, alipofikishwa baada ya kufunguliwa kesi ya madai namba 29/2013 na mabosi wa Clouds Media Group, Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga.
         Hali katika mahakama hiyo iligubikwa na huzuni baada ya watu kumuona Lady Jaydee akiwasili eneo hilo sambamba na mumewe Gadner G Habash ambapo walifananishwa na wanandoa mastaa wa Marekani, Shawn Carter ‘Jay Z’ na Beyonce Giselle Knowles, walipotimba mishale ya saa 6:00 mchana.
Risasi Mchanganyiko liliwashuhudia mastaa hao wakiingia eneo hilo huku wakiwekewa ulinzi mkali kama ilivyo kawaida mahakamani kuhakikisha usalama wa watu.
Wawili hao waliongozana hadi chumba cha makarani ambapo walielezwa kesi inayomkabili mwanamuziki huyo na kupangiwa siku ya kesi ambayo ni Mei 27, mwaka huu.
Pia walitajiwa hakimu atakayeendesha kesi yao kuwa ni Athumani Nyamrani wa chumba namba 2 cha mahakama hiyo.
Baada ya kupewa utaratibu wa kesi hiyo walichomoka mahakamani na ndipo wakakutana na paparazi wetu aliyewasimamisha na kutaka kujua madai yaliyofunguliwa.
           JAYDEE AAHIDI KUPAMBANA
Akizungumza na paparazi wetu, Lady Jaydee alisema: “Kesi inahusiana na masuala ya kimtandao, eti Ruge na Kusaga wanadai nimewachafua.
“Kwa leo sitaki kusema mengi, baada ya kupata fomu hizi sasa hivi tunampelekea mwanasheria wetu lakini kila kitu kitawekwa bayana Mei 27, kesi itakapotajwa mbele ya hakimu.
“Kama wameamua kupambana na mimi nitapambana kwa msaada wa Mungu.”
                    HOFU YA KUFILISIWA
Baadhi ya watu waliokuwa mahakamani hapo walionekana kumuonea huruma mwanamuziki huyo kwa jinsi alivyokuwa akihenya kwenye viunga vya mahakama hiyo huku akipishana na askari wenye silaha nzito.
                 Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo alisikika akisema kesi hiyo inaweza kumpotezea muda mwingi na kumuathiri kisaikolojia kwani haijulikani hatima yake ni nini.

No comments: